
Machi/2025 - Mei/2025

Machi/2025 - Mei/2025
S.L.P. 2696, Arusha 0759 544 917
Barua pepe: editor.somabiblia@gmail.com
Kamati ya Riziki:
Mch. Elitegemeo Y. Mpumpa (mhariri)
Mch. Anza Amen Lema
Mch. Philip Bach-Svendsen
Cathbert Msemo
Mary Bura
Magreth Mushi
Mch. Gervas Meitamei Luhekelo Sanga
Waandishi walioshiriki:
Mch. Gideon Mumo Bertha Chris
Layout: Cathbert Msemo
Jalada: Cathbert Msemo
ISSN 2683 - 6491
Nakala: 5000
Usambazaji: SOMA BIBLIA
S.L.P. 2696, Arusha
S.L.P. 12772, Dar es Salaam
S.L.P. 1088, Iringa
S.L.P. 6097, Mwanza
S.L.P. 1062, Mbeya
S.L.P. 4231, Dodoma
www.somabiblia.or.tz
Neno la Injili
kwa rika zote
Tanzania!
Imechapwa na: Imaging Smart Dar es Salaam
Je, umewahi kujikuta katika hitaji kubwa la kuomba ulinzi wa gari lako kiasi kwamba ulitumia damu ya Yesu katika maombi yako? Wakati kama huo ulihofia nini? Na ulikuwa unaona nini mbele yako?
Katika maisha haya watu wengi wanatumia damu ya Yesu kwa mambo mengi. Lakini je, matumizi haya yote ni sawa?
Soma makala ya “Kwa damu ya Yesu” ili kutafakari swali hili zaidi.
Wakati viongozi wa kiyahudi walipompeleka Yesu kwa Pilato, na huyu aliona Yesu ni mwenye haki na hastahili kufa, walimjibu Pilato, “Damu yake na iwe juu yetu, na juu ya watoto wetu” (Mt 27:25). Hili ni ombi baya sana, lakini hukumu hii ni tokeo lake ikiwa tunakataa matumizi halisi ya damu ya Yesu, yaani jinsi yeye mwenyewe alivyofanya upatanisho kwa njia ya kifo chake.
Soma pia makala kuhusu Paulo na anavyosema kwamba neema ya Mungu yamtosha. Ushuhuda huu hutokana na Paulo alivyoona kwamba damu ya Yesu inanena mema kuliko damu nyingine zote zilizomwagwa hapa duniani tangu Kaini alipomwua ndugu yake. Tumshukuru Mungu kwamba katika neema yake ametufungulia chemchemi ya kutakasa dhambi kwa njia ya damu ya Yesu.
Utapata pia kusoma mada kuhusu damu ya Yesu ilivyo na maana kwa ushirika wetu kama Wakristo, na ushuhuda wa kukutia moyo wakati unapoona ni kana kwamba Mungu hasikii maombi yako ya muda mrefu.
“This car is protected by the blood of Jesus”. Bila shaka umewahi kuona maandishi haya yakiwa yamebandikwa kwenye gari. Sisi sote twajua ajali nyingi hutokea barabarani. Kwa hiyo mwenye gari hilo ameweka chombo chake chenye thamani mikononi mwa Mungu kwa njia ya maombi, na kuonesha imani yake katika ulinzi wa Mungu kwa kubandika ujumbe huo kwenye gari.
Pengine alitumia pia maneno haya alipolifanyia maombi? Wengi huongeza
“kwa damu ya Yesu” wanapoombea jambo fulani, tena wanayatamka maneno haya kwa msisitizo mkubwa, huenda wakiyarudia mara kadhaa.
Kwa nini? Je, sababu ni kama mwandishi wa kitabu fulani alivyoeleza kuhusu maombi, kwamba usipojibiwa kwa namna nyingine, basi tumia kuomba kwa damu ya Yesu, maana maombi haya yana uhakika zaidi? Tusemeje kuhusu maoni na matumizi hayo?
Maana ya damu
Ni muhimu kupima yote kwa kuangalia
Neno la Mungu lasema nini.
Uk. 3-6: Kwa damu ya Yesu
Mch. Elitegemeo Y. Mpumpa
Uk. 7-8: Mtume Paulo: Neema yanitosha!
Uk. 9-10: Jumuiya kama ushirika mdogo wa kikristo
Uk. 11-12: Imefunguliwa chemchemi ya kutakasa dhambi
Uk. 13-14: Magumu yasikutoe katika kumpenda Mungu
Uk. 15: Vitabu viwili unavyohitaji kuvisoma!
Mambo ya Walawi 17 ni mlango muhimu kuhusu maana ya damu na matumizi yake. Unaanza na sharti kwamba machinjo yote yatakiwa kufanyika kwenye hema ya kukutania. Baadaye, Waisraeli walipoanza kukaa sehemu mbalimbali za Kana’ani, sheria hii ilibatilishwa, lakini maana na matumizi ya damu yalidumu.
Sababu ipo katika mst.14: “Uhai wa wanyama wote ni katika hiyo damu yake”. Pia mwanadamu ni mhusika. “Damu yake
ni moja na uhai wake”. Kwa sababu Mungu ndiye Muumba na Mhifadhi wa uhai wote, damu ni mali yake. Ndiye bwana wa damu anayeamua ni wapi na lini maisha ya kiumbe hai yataisha. Kuna sababu nyingine pia ya sharti hilo: Liwalinde Waisraeli dhidi ya ibada ya sanamu. Kama watu wote, wao pia waliuliza mwanadamu anapaswa kufanya nini anapotambua kwamba amemkosea Mungu. Jibu ni kwamba lazima upatanisho ufanyike! Katika dini na tamaduni nyingine dhabihu za wanyama zilitumika kwa lengo la kumtuliza mungu mwenye hasira.
Lakini njia hii haifai, hata kidogo. Katika mst.11 Mungu anaonesha kwamba upatanisho wa kweli kati yake na mwanadamu wapatikana kwa njia tofauti kabisa. Njia ndiyo hii moja: “Uhai wa mwili u katika hiyo damu; nami nimewapa ninyi hiyo damu juu ya madhabahu, ili kufanya upatanisho kwa ajili ya nafsi zenu; kwani ni hiyo damu ifanyayo upatanisho kwa sababu ya nafsi.”
Zingatia neno hili “nami nimewapa”. Mwanzilishi wa upatanisho ndiye Mungu. Ndiye pia mtoaji. Katika neema yake ametufungulia njia ambayo kwayo dhambi na hatia vyaweza kuondolewa kati yake na sisi wenye dhambi, ili kuturudisha kuwa watu wake naye awe Mungu wetu. Damu imetengwa kwa ajili ya kusudi hili maalumu, na mtoaji ndiye Mungu mwenyewe!
Mungu alivyotoa damu yake Kwa hiyo Paulo anaweza kuwaambia Wakristo wa Efeso kwamba Mungu alilinunua kanisa lake “kwa damu yake
mwenyewe” (Mdo 20:28). Katika barua ile aliyowaandikia, anaeleza zaidi jinsi ilivyotukia. Katika Yesu Kristo, kwa damu yake, tunao ukombozi wetu, masamaha ya dhambi, sawasawa na wingi wa neema yake Mungu (Efe 1:7). “Ninyi mliokuwa mbali hapo kwanza mmekuwa karibu kwa damu yake Kristo” (Efe 2:13).
Damu ya mbuzi na mafahali haiwezi kuondoa dhambi. Hata hivyo dhabihu zilizotolewa kipindi cha Agano la Kale zilikuwa na maana kubwa. Zilikumbusha dhambi na kuwa mfano wa jinsi Yesu, kama kuhani mkuu, alivyoingia mbinguni hasa kwa damu yake mwenyewe na kupata ukombozi wa milele kwa ajili yetu (Ebr 9:11-14).
Ishara ya uhai au kifo?
Waisraeli walikatazwa kabisa kula damu “kwa kuwa uhai wa mwili u katika hiyo damu”, hata damu “ni moja na” uhai (Law 17:11, 14). Je, habari hiyo ina maana gani kwa damu ya Yesu? Wengi husema
Picha: freeimages.com
kwamba Yesu alimwaga damu yake msalabani. Mwenyewe alisema kwamba alitoa uhai wake kwa ajili yetu (Yn 10:11). Je, hiyo inamaanisha kwamba damu ya Yesu ni nguvu ya uhai tunayoweza kuipokea kutoka kwake na kuitumia, kidogo kama vile mtu awezavyo kuvuna utomvu kwenye mti?
Yaonekana hilo ni wazo la msingi katika mafundisho mengine kuhusu maombi. Husema kwamba damu ya Yesu inaongelea uhai au uzima wake katika ufufuo. Kwa hiyo ina uzima ndani yake. Ukiikiri katika maombi yako na kuamini uzima uliomo, utabadili maisha yako na utapata matokeo chanya.
Wapo wanaounganisha dhana hiyo na meza ya Bwana, wakituambia, “Kunywa kwa imani, kisha kwa hiyo damu ndani yako kiri kuwa inatenda kazi. Nguvu yake damu ya Yesu itanifanya nifanikiwe katika maisha.”
Mafundisho hayo tunaweza kuyajumlisha kwa namna hii: Jinsi damu ya Mwa-
na-kondoo Yesu Kristo ilivyotupatia mafanikio ya kiroho katika ulimwengu wa kiroho, ndivyo Mkristo anavyotakiwa kujipatia mafanikio ya kimwili katika maisha haya kwa kuinyunyizia damu hiyo kwenye sehemu zote za maisha yake kwa njia ya maombi ya kuugua na imani katika anachokifanya.
Tukichunguza Biblia inasemaje, hatuna budi kukataa mafundisho hayo juu ya damu ya Yesu kama nguvu ya uhai. Biblia inapoongelea damu yake inamaanisha kifo cha Yesu. Mwandishi wa Waraka kwa Waebrania anasema kwamba Yesu “alijitoa nafsi yake kwa Mungu kuwa sadaka”, na kuendelea kulifafanua tendo hili kama “mauti” iliyofanyika kwa ajili ya kukomboa makosa (Ebr 9:14-15). Angalia pia mst.22 ilipoandikwa kwamba “pasipo kumwaga damu hakuna ondoleo”. Maneno kama haya yadhihirisha kwamba damu ya Yesu humaanisha kifo chake, na kwamba kifo hicho kilifungamana na hukumu ya Mungu juu ya dhambi. Yesu alikufa badala yetu kama tokeo la yeye kuchukua dhambi zetu juu yake, na pamoja na dhambi zetu pia hukumu yetu ya kifo.
Kwa sababu Yesu ni Mwana-kondoo wa Mungu, tunaweza kulinganisha maana ya damu yake na damu ya mwana-kondoo wa pasaka. Mungu alitangaza kifo cha kila mzaliwa wa kwanza nchini kote kama hukumu yake juu ya Misri. Kwa usiku mmoja wazaliwa wote walikufa, isipokuwa wale waliokaa ndani ya nyumba yenye damu ya mwana-kondoo katika miimo miwili ya mlango na katika kizingiti cha juu.
Asubuhi walitoka wakiwa hai. Kwa nini?
“Ile damu itakuwa ishara kwenu”, Mungu anaeleza. Maana yake, itakuwa ishara ya
kwamba kifo kimeshafanyika. Kwa hiyo Mungu anaendelea kusema, “Nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu, lisiwapate pigo lo lote likawaharibu, nitakapoipiga nchi ya Misri” (Kut 12:13).
Yesu alipoanzisha chakula chake, alikiunganisha na tukio hilo la pasaka ya kwanza. Na alifafanua maana ya damu yake kwa kusema kuhusu divai kwamba “ndiyo damu yangu ya agano” (Mt 26:28). Damu yake, ambayo yaashiria kifo chake cha upatanisho, ni msingi wa agano jipya ambalo kwalo sisi tunaweza kumkaribia Mungu na kuishi naye kama watoto wapendwa wa baba yao. Maana “hakuna hukumu ya adhabu juu yao walio katika Kristo Yesu” (Rum 8:1).
Matumizi ya damu ya Yesu Natumaini ni wazi kwamba damu ya Yesu si kitu tunachoweza kukitumia sisi kama fidia tunayomrudishia Mungu yenye uwezo wa kuondoa mafarakano kati yake na sisi. Alikosa kabisa maana yake, mtu yule aliyeandika kwamba “tunapaingia Patakatifu pa Patakatifu kwa damu ya Yesu kwa imani ili kufanya upatanisho na Mungu”. Upatanisho huo umeshafanyika, na mtendaji wake alikuwa ndiye Mungu, Yesu alipoingia mbinguni kwa damu yake mwenyewe na kupata ukombozi wa milele.
Lakini hata hapa duniani damu ya Yesu haina matumizi tena! Siyo kwamba kunywa damu yake kwa imani kwenye meza ya Bwana kunatutia nguvu ya uhai ndani yetu tusiwe wagonjwa wala kufa. Vilevile damu ya Yesu siyo nguvu tunayoweza kuitumia kwa kufanikisha matakwa yetu. Kwa mfano, yule anayezungumza juu ya “tone la damu ya Yesu” na nguvu yake
ya kutufanikisha hivyo, hajaelewa kabisa maana yake. Sisi hatuwezi “kuimimina” au “kuinyunyiza” damu ya Yesu juu ya kitu chochote, kwa mfano gari letu. Hakuna gari lolote lililolindwa na damu ya Yesu. Lakini huenda dereva wake amelindwa nayo. Ndivyo alivyo ikiwa amekubali kupatanishwa na Mungu kwa kupokea kwa imani habari njema kwamba “Mungu alikuwa ndani ya Kristo, akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake” (2 Kor 5:18-20).
Vilevile siyo kweli kama mmoja alivyoshauri kwamba “unapohisi ugonjwa wowote ule au giza lolote katika maisha yako, itumie damu ya Yesu kujitakasa mbali na dhambi pamoja na laana zote ikiwemo magonjwa, nawe utakuwa huru kweli kweli”. Badala yake, tumshukuru Mungu kwa ukombozi huo wa milele uliotokana na Yesu kuingia mbinguni kwa damu yake ya upatanisho.
Damu inenayo mema
Wakati huu, maana ya damu ya Yesu kwa maombi yetu ni kwamba tunaweza kukikaribia “kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji” (Ebr 4:16). Ujasiri huu watokana na kwamba damu ya Yesu ya upatanisho imefanya kiti cha
hukumu cha Mungu kuwa kiti cha neema.
Na tukifikiri juu ya wakati ujao, yaani kuhusu siku ya mwisho ambapo sisi sote tutadhihirishwa mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo, maana ya damu ya Yesu ni waumini wote kuachiliwa huru. Maana “tukiisha kuhesabiwa haki katika damu” ya Yesu kwa kumwamini kuwa ndiye “kipatanisho kwa dhambi zetu” (1 Yoh 2:2), “tutaokolewa na ghadhabu kwa yeye” (Rum 5:9).
Basi, tujitahidi kuacha kutumia “kwa damu ya Yesu” katika kuomba kwetu kana kwamba tungeweza kuhakikisha mafanikio ya maombi yetu kwa njia ya kuyatamka maneno hayo. Vilevile tuache lugha hii ya “kuinyunyiza damu ya Yesu” juu ya hiki na kile, maana lugha hiyo hufungamana na imani isiyo ya kibiblia. Badala yake, tumwombe Mungu kwa ujasiri kama watoto wanaojua kwamba baba yao anawapenda sana. Haijalishi kama tukiyaona mambo ya maisha yetu kuwa mema au mabaya, Mungu anatenda kazi katika hayo yote, na mwisho wake utakuwa mema, maana Yesu aliingia kwa damu yake mwenyewe mara moja tu katika Patakatifu pa mbinguni na kutupatia ukombozi wa milele (Rum 8:28, Ebr 9:12).
Mch. Philip Bach-Svendsen
Kuna silaha mbili anazozitumia Shetani dhidi ya wafuasi wa Kristo, tena kwa ushindi mkubwa, na hasa kwa walio na historia ya kujivunia jinsi walivyokutana na Mungu, na jinsi Mungu anavyowatumia kwa njia ya kipekee kwa huduma.
Silaha ya kwanza ni kiburi. Na ya pili ni kutufanya tushuku upendo wa Mungu kwetu - hasa tunapojikuta kwenye dhiki na mateso licha ya kumtumikia Mungu kwa uaminifu.
Je, tufanye nini tunapojikuta kwenye mtego huu? Naomba tujifunze kutoka kwa maisha ya Mtume Paulo.
Ushuhuda mzito
Kawaida uzito wa ushuhuda wa jinsi tulivyokutana na Yesu unawiana kwa karibu sana na kina cha shimo tulimotolewa.
Hivyo mchawi atajivunia kuwa na ushuhuda mzito, tena wa kusisimua, kuliko ushuhuda wa mtu aliyekuwa kanisani tangu utoto, ila hakumpokea Yesu hadi alipokuwa mtu mzima. Lakini hebu sikiliza sifa za ushuhuda wake Mtume Paulo, aliyeitwa Sauli kabla ya kuongoka.
Paulo anajitambua kuwa mwenye dhambi nambari moja: Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa, ya kwamba Kristo Yesu alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi; ambao wa kwanza wao ni mimi (1 Tim 1:15).
Sababu yake kuu ni jinsi alivyowaudhi Wakristo. Kwa kabila alikuwa Myahudi aliyesoma sheria zote za dini chini ya Gamalieli, mwalimu mkuu wa sheria siku zile (Mdo 22:3). Hivyo alihitimu kutambua kila fundisho lililokuwa kinyume na sheria za dini ya kiyahudi. Kwa jitihada
za kidini aliomba kupewa kazi ya kuwaudhi wafuasi wa Kristo kwa kuwatafuta, kuwatia gerezani, na hata kuwaua (22:4). Akiwa kijana alikuwa kwa kundi lililompiga Stefano mawe (7:58).
Mtukanaji anakuwa mfuasi Tukirudi kwa alivyoongoka, Paulo ana ushuhuda wa kusisimua kuliko wengi wetu. Akiwa anaelekea Dameski kuwakamata na kuwaleta wafuasi wa Kristo Yerusalemu ili waadhibiwe, ghafla nuru ya Yesu ilimwangaza kutoka mbinguni. Hapo alianguka, na Yesu akamwita kutoka juu mbinguni, “Sauli, Sauli, mbona wanihudhi?” (9:3-4).
Alipofumbua macho, kumbe alikuwa amepigwa na upofu. Watumishi wake walimshika mkono na kumwongoza hata Dameski. Kwa siku tatu hakuona, hakula wala kunywa (9:5-9). Baada ya siku hizo tatu Paulo aliombewa na mwanafunzi wa Yesu aitwaye Anania. Hapo akaponywa macho, akala, akanywa, akabatizwa, na moyoni akabadilishwa kutoka mtesaji wa wafuasi wa Yesu hadi kuwa mhubiri hodari wa Injili ya Kristo (9:18-20, 22). Paulo alitembea na kusafiri kwa meli kwa kazi ya Injili kuliko Misionari mwingine awaye yote. Nyaraka alizoandika, wakati mwingine akiwa gerezani, kwa makanisa na kwa watu binafsi ni ushuhuda wa jinsi alivyojitoa na kufanikiwa kwa kazi ya Mungu.
Kuteswa kwa ajili ya Yesu
Sasa je, si kwamba wengi waona kuna ufahari mkubwa kwa mhubiri kupokea maono na mafunuo maalumu kutoka mbi-
nguni? Mtume Paul angejisifu hata zaidi. Maana anashuhudia kunyakuliwa hadi mbingu ya tatu na kupata mafunuo ambayo lugha ya wanadamu haiwezi kuyaelezea (2 Kor 12:1-4).
Kwa kweli maisha ya Mtume Paulo yalimpa nafasi nzuri ya kujisifu na kutazamia thawabu ya kipekee kutoka kwa Mungu na kwa watu. Lakini kinyume na matarajio yetu kwa mtu kama huyu, mji baada ya mji vifungo na dhiki vilikuwa vyamgoja (Mdo 20:23). Maana alitekwa nyara (21:27), mara kadhaa alipigwa (21:30-31; 23;3), alikamatwa mara kadhaa (21:33; 22:24,31; 23:35; 28:16), alishitakiwa mbele ya wakuu (21:34; 22:30; 24:1-2; 25:2,7; 28:4), alihojiwa (25:24-27), alidharauliwa (27:11), karibu afe maji (27:41), aliumwa na nyoka (28:3) n.k. Na ingawa Biblia haijanukuu, inaaminika kwamba Mtume Paulo aliuawa kwa sababu ya imani na kazi yake ya Injili.
Kamwe Mungu hakumtunuku maisha ya raha kwenye utumishi wake. Paulo alijua kudhiliwa na kupungukiwa. Ni wa pekee, ambaye zaidi ya kutokuwa na familia ya kutegemea hakutaka kulemea makanisa aliyoyaanzisha. Kwa mikono yake alifanya kazi kutosheleza mahitaji yake na ya wengine (Mdo 20:34).
“Nisipate kujivuna”
Sawa na watu wengine, Paulo pia aliugua. Anashuhudia kupata ugonjwa uliomsumbua kwa miaka mingi (2 Kor 12:7).
Tena inashangaza kwamba yeye ambaye kwa mkono wake Mungu alifanya “miujiza ya kupita kawaida” (Mdo 19:11), hakupata muujiza wa kupona mwenywe,
ingawa alimsihi Mungu mara tatu (2 Kor 12:8)! Mbona?
Licha ya kuwa na kila sababu ya kujisifu kwa maisha na jinsi Mungu alivyomtumia kwa kazi ya Injili, Paulo alinyimwa maisha ambayo yangemletea kiburi. Hakuweza kujisifu kwa wokovu, aliokolewa na neema tu. Hakuweza kujisifu kwa familia, hata hakuwa na mke. Hakuweza kujisifu kwa mshahara mkubwa, alikula kutoka kwa mikono yake mwenyewe. Hakuweza kujisifu kwa afya nzuri, alikuwa na ugonjwa usiopona. Wala hakuweza kujisifu kwa mafanikio ya kazi ya Injili, maana ni katika udhaifu wake kwamba Mungu alidhihirisha uweza wake (2 Kor 12:9).
Neema ilizidi sana
Je, kumebaki nini cha kujivunia kwa maisha na mafanikio yetu? Naomba mimi na wewe tufikie uelewa wa Mtume Paulo wa kuridhika kubaki chini ili yeye Kristo ainuliwe. Maana yake, tubaki chini ya neema ya Mungu ili Kristo Yesu apate kuidhihirisha neema yake hiyo, watu wengi wapate kuiona na kuipokea na hivyo kuwa na uzima wa milele (rudia 1 Tim 1:15 ukitafakari pia mst.16). Naomba Mungu atujalie neema ya kukubali hali yoyote ile mradi itamletea Kristo sifa. Naomba kwamba mengine yote yakipotea, itabaki kwetu ibada iliyojengwa kwa imani inayomwambia Mungu: “Neema yako yanitosha” (2 Kor 12:9).
Jumuiya kama ushirika mdogo wa kikristo
Mch. Gideon Mumo
Katika ulimwengu wa sasa, mawasiliano mengi yanafanyika kwa njia ya mitandao bila watu kuonana. Kwa upande wa makanisa, sharika nyingi ni kubwa, hata ni lazima kuwa na ibada mbili au tatu kila Jumapili ili wote wapate nafasi ya kuhudhuria.
Wakati ni raha kuweza kupiga simu kwa mtu ambaye hatujamwona muda mrefu, na ni furaha kuona jinsi majengo mengi ya kanisa yalivyojaa watu wengi wanaotaka kumwabudu Mungu, hali hii ina changamoto zake pia. Jinsi gani mchungaji ataweza kuwa karibu na kila mmoja kwa mafundisho na ushauri? Jinsi gani tunaweza kufuata mwongozo katika
1 Kor 14:26 unaosema kwamba “mkutanapo pamoja, kila mmoja ana zaburi, ana fundisho”, n.k.?
Jumuiya inavyojibu haja zetu
Sehemu ya jibu inaweza kuwa ibada za jumuiya. Hapo watu si wengi, na wanapata kusalimiana, kuongea kidogo na kufahamiana zaidi. Kwa sababu wametoka sehemu moja ndogo ya eneo kubwa la usharika, wanaweza kubahatika kuonana siku nyingine pia ya juma, na kupita kwa yule ambaye hakufika ibadani ili kumsalimia na kuona kama yuko salama au pengine ni mgonjwa na anahitaji msaada. Katika usharika mkubwa ni rahisi kwa mtu kuacha kushiriki ibada bila wengine kugundua. Si hivyo katika ushirika wa jumuiya ambapo wote wanafahamiana na kuwa na mazoea ya kushirikiana mambo ya kila siku kwenye ibada za pamoja.
Kuwa karibu kivitendo
Ushirika mdogo wa Kikristo una uwezakano wa kuleta faida kubwa kwa washiriki wake.
Paulo anasema kwamba “katika Kristo Yesu, ninyi mliokuwa mbali hapo kwanza mmekuwa karibu kwa damu yake Kristo” (Efe 2:13). Maana yake ya kwanza ni kwamba hao waliokuwa “hamna tumaini, hamna Mungu duniani”, sasa wamekuwa wana wake wapendwa. Lakini upatanisho wa Yesu umewaletea ushirika mwingine pia. Wamekuwa karibu wao kwa wao (soma Efe 2:14-19).
Ushirika huu ni muhimu kwa Wakristo wote, na ibada za jumuiya huwapa kuoneshana umoja huo katika Kristo na ushirikiano wa karibu kwa vitendo. Ila inabidi ibada hizi zisiwe tu kama ‘ibada ndogo’ inayofuata kamili utaratibu wa ibada za kanisani. Ziandaliwe ili iwepo nafasi nzuri kwa wanaohudhuria kusikilizana, kuombeana na kushauriana. Kusoma Neno la Mungu pamoja, maana yake siyo mahubiri ya mtu mmoja, bali hutoa nafasi ya kuuliza maswali, kujadiliana yaliyosomeka kama ndugu, kutoa ushuhuda wa jinsi neno hilo lilivyokusaidia n.k. Hivyo wote wanachangia kwa kutiana moyo, kuimarishana kiroho na kusaidiana kuepuka kuyumbishwa kiimani na dini au madhehebu yanayozuka. Kujengana imani na kuchukuliana mizigo ya ugumu wa maisha namna hii ni kuoneshana upendo mkuu. Pengine hakuna upendo mkubwa zaidi miongoni mwa Wakristo? Na siyo tu kwamba wa-
nasaidiwa wenyewe kuimarika kiroho, hata wasio Wakristo wanaweza kuvutwa kushiriki.
Jumuiya kama kundi dogo la uinjilisti
Ushirika mdogo wa jumuiya unaweza kuchangia katika kuimarisha jamii nzima kwa jumla. Huweza kuleta motisha maradufu. Kwa upande wa wanajumuiya wenyewe, wanapokutana na kushirikiana mara kwa mara, wanajenga utamaduni wa kusaidiana na kuwa na malengo ya pamoja. Huweza kuchochea moyo wa kuwasaidia hata wasio Wakristo na kuwakaribisha kwenye jumuiya. Kwa upande wa wasio Wakristo, tuna haja moja nao ya kihisia na kimaisha. Sisi sote tunavutwa kushiriki tukiona ushirika wenye umoja wa upendo na mshikamano wa kivitendo. Pengine kwanza wanafikiri tu juu ya wanajumuiya wanavyochukuliana magumu ya maisha ya kila siku, lakini wakianza kuhudhuria ibada za jumuiya
Picha: freeimages.com
watajifunza pia kupenda jinsi Wakristo wanavyoshirikiana mambo ya kiroho, kuombeana n.k.
Hivyo ushirika mdogo wa jumuiya hupata kuwa mlango wa kuingia katika usharika mkubwa kanisani.
Tusiache kukusanyika pamoja
Neno la Mungu linatukumbusha kuangaliana sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri (Ebr 10:2425). Tumeona jinsi ushirika mdogo wa jumuiya unavyoweza kuwa chombo kizuri katika kufikia lengo hili. Basi, tutafute kushiriki katika ibada hizi na pia kuwakaribisha wengine kufurahia faida zake pamoja nasi.
Na ikiwa hakuna jumuiya ya Kikristo pale unapokaa? Basi, ongea na Mchungaji wako, au jirani yako Mkristo, kama mtaweza kuianzisha. Karibu pia kuwasiliana na mhariri wa Riziki aliyeandika makala hii.
Mch. Elitegemeo Y. Mpumpa
Nyimbo nyingi tunaziimba na kuzifurahia. Lakini tukipata kutafakari maneno yake, tunaweza kutamani kujua hata zaidi juu ya kilichotokea mpaka wimbo huo ukatungwa.
Katika makala hii nitaeleza kwa ufupi historia ya William Cowper, mtunzi wa “Damu imebubujika” (Tenzi za Rohoni na. 86; Praise for the Fountain Opened kwa Kiingereza, with the first line saying, There is a fountain filled with blood).
William Cowper alizaliwa huko
Berkhamsted, Hertfordshire, Uingereza mwaka 1731. Baba yake aliishi kama mkuu wa Kanisa la Mtakatifu Petro. William alipokuwa na umri mdogo wa miaka sita, mama yake alifariki wakati wa kujifungua. Kifo cha mama yake kilimwathari sana mtoto William. Alipata msongo mkali wa mawazo, na hali hii ya kiakili ilimfuata maisha yake yote.
Shuleni William Cowper alikuwa na uwezo. Alisoma Kilatini na uandishi wa mashairi, na baadaye pia taaluma ya sheria, lakini hakupata nafasi ya kufanyia kazi taaluma yake kama wakili.
Wakati fulani akiishi kwa mjomba wake alipendana na binamu yake aliyeitwa Theodora. William alitaka kumwoa, lakini baba yake alikataa uhusiano wao.
Katazo hili lilihuisha tena hali hiyo yenye msongo wa mawazo, kiasi kwamba alijaribu kujiua mara tatu, na karibu angefaulu.
Wakati huu alipelekwa katika hospitali ya vichaa.
Lililomsaidia William Cowper ni kwamba alipewa hifadhi chini ya uangalizi wa Dk. Cotton, daktari Mkristo.
Wakati wa kukaa kwake kwa miezi 18, alianza kusoma Biblia. Ilileta amani akilini na rohoni mwake, na hatimaye akapata nafuu.
Kisha William Cowper alihamia Olney na kuishi nyumbani kwa Morley Unwin, mchungaji mstaafu. Huko alikutana na mwandishi wa nyimbo John Newton na kuanza kumsaidia katika kazi zake za kichungaji.
Newton alimwalika Cowper kuchangia katika kitabu cha nyimbo alichokuwa akitunga kiitwacho Olney Hymns. Mwaliko huu ulimpa Cowper mwamko mkubwa, na alichangia nyimbo nyingi ikiwemo “Damu imebubujika”. Nyimbo zake aliziandika kama shukrani kwa Mungu aliyemwokoa wakati alipojaribu kujiua. Cowper alistawi chini ya uongozi wa Newton huko Olney, na alikuwa na vipindi vya furaha zaidi maishani mwake. Hata hivyo, alipopokea habari za kifo cha kaka yake, alijisikia kana kwamba Mungu alimwekea hukumu ya Jehanamu na kutaka atoe maisha yake, na hivyo alijaribu tena kujiua. Aliugua na kuhangaika kwa muda wa miezi 16. Muda wote aliishi katika nyumba ya Newton, na Mary Unwin, mjane wa Morley Unwin, alijitolea kumtunza.
William Cowper na Mary Unwin wakawa rafiki wa karibu. Kwa hiyo, Mary alipokufa mwaka 1796, hali hiyo ya Cowper kuugua kwa msongo mzito wa mawazo ilirudi tena na kumtumbukiza kwenye giza ambalo hakupona kabisa. Hivyo alifariki mwaka 1800 na kuzikwa katika kanisa la Mtakatifu Thomas Canterbury.
Wimbo huo “Damu imebubujika” ni tafakari juu ya uwezo wa kuokoa wa damu ya Yesu. Inasemekana kuwa William Cowper aliuandika wakati akitafakari juu ya Zakaria 13:1, “Katika siku hiyo, chemchemi itafunguliwa kwa nyumba
ya Daudi na wakazi wa Yerusalemu, kuwatakasa dhambi na unajisi”. Karibu tuimbe pamoja wimbo huu tukitafakari jinsi damu ya Yesu inavyotutakasa maovu yetu.
Cathbert Msemo
1. Damu imebubujika, ni ya Imanweli, Wakioga wenye taka, husafiwa kweli.
2. Ilimpa kushukuru mwivi mautini; Nami nisiye udhuru, yanisafi ndani.
3. Kondoo wa kuuawa, damu ina nguvu, Wako wote kuokoa, kwa utimilivu.
4. Bwana tangu damu yako kunisafi kale, Nimeimba sifa zako; taimba milele.
5. Nikifa tazidi kwimba sifa za wokovu
Ulimi ujaponyamaa vumbini mwa ufu.
6. Bwana, umenikirimu nisiyestahili Kwa damu yako, sehemu ya mali ya kweli.
7. Nikubali kukwimbia, mbinguni milele, Mungu nitakusifia Jina lako pweke.
Niliolewa miaka 16 iliyopita na mwanaume wa chaguo langu, nikiwa na umri wa miaka 27. Katika kipindi chote cha ndoa yetu amekuwa nguzo muhimu katika maisha yangu.
Mume wangu ni mtoto wa pekee katika familia yao. Kuolewa kwangu katika familia yao kuliongeza furaha kubwa kwa wazazi wake, maana waliona wameongezewa mtoto katika familia yao. Wamekuwa wakinipenda sana kabla na baada ya kuolewa. Wamekuwa washauri wangu na mume wangu kwa muda mrefu.
Nilitokea katika familia ambayo mama yangu ni mjane baada ya baba yangu kufariki nikiwa na miaka 12 tu. Kwa hiyo, kuolewa katika familia ambayo baba mkwe na mama mkwe wananipenda sana, kulihuisha na kuongeza furaha yangu ya kuishi bila baba kwa miaka yote hiyo.
Pamoja na kuishi na wakwe wanaonipenda kuliko ninavyoweza kueleza, mimi na mume wangu tumekuwa na changamoto ya kupata watoto. Kila familia hutazamia uzao mara tu baada ya kuoana, lakini haikutokea hivyo kwetu.
Tulijaribu mara nyingi kupata mtoto, tukipita kwenye mikono ya matabibu wengi na kupata ushauri toka kwa wataalamu wengi. Lakini hatukufanikiwa.
Hali hii ilitutesa sana. Japo mume wangu alikuwa haoneshi kwa nje hali ya kuumia, nilikuwa najua wazi kuwa kwa ndani alikuwa anaumia sana. Ila alificha hivi ili kunilinda mimi. Hata wakwe zangu hawakuonesha hali yoyote ya kunisema au kunichukia kwa sababu ya kutokupata mtoto. Unajua katika jamii yetu ya
kiafrika, mwanamke ndiye wa kubeba lawama zote pale ambapo familia inakosa mtoto.
Kwa upande wa mama yangu hali ilikuwa tofauti. Kila mara nilipokutana naye, cha kwanza alichokuwa ananiuliza ni lini tutamletea mjukuu. Swali hili si tu kwamba lilikuwa linanikera, hata lilikuwa kama kisu kilichokuwa kinapita ndani ya moyo wangu. Maumivu yake yalikuwa makali sana, japo nilikuwa najikaza kutokuonesha kwa nje maumivu yake. Mara zote nilimwambia mama, “Mungu ndiye anayetoa watoto. Jambo hili lingekuwa mikononi mwangu, ningekuwa nimeshakuletea wajukuu, Mama.”
Katika hali hii jambo moja ambalo mume wangu alikuwa ananitia moyoni kila mara, ni imani katika Mungu juu ya Yeye kutupatia uzao siku moja. Kila mara tulipokuwa katika kuomba, alikuwa anamshukuru Mungu kwa ahadi ya uzao. Kila mara alikuwa anakiri kuwa katika wakati na majira ya Mungu tutapata mtoto.
Katika kushauriana na kutafuta ushauri kwa matabibu, siku moja tukiwa kliniki kuonana na mtaalamu wa masuala ya uzazi, alituambia kuwa anaona daktari fulani kutoka Afrika Kusini, bingwa wa masuala ya uzazi, ataweza kutusaidia. Mara baada ya kusikia jambo hili niliiona imani ya mume wangu ilivyoongezeka maradufu kuwa tutafanikiwa kupata mtoto. Kumbuka tumeishi miaka 15 sasa bila mtoto. Tulipewa mawasiliano ya tabibu huyu, na mara moja tulianza kuwasiliana naye akiwa nchini kwao Afrika ya Kusini. Ali-
tusikiliza na kutushauri kupanga safari ya kwenda kumwona nchini Afrika Kusini katika jiji la Pretoria. Tulifanya kila lililo ndani ya uwezo wetu kupata fedha kwa ajili ya kwenda kumwona. Hata tulipowashirikisha wazazi wetu na hasa baba mkwe, walikuwa tayari kutupa fedha kwa ajili ya kusafiri kwenda Afrika Kusini. Huyu baba ndiye aliyetulipia tiketi ya ndege ya kwenda na kurudi Afrika Kusini. Pia alitulipia hoteli na gharama nyingine ambazo zilitusaidia kuishi kule kwa muda wa miezi miwili na nusu.
Kabla ya kusafiri tuliwaita rafiki zetu wachache ambao tulikuwa tunashirikiana nao tukiombea mambo mbalimbali. Tuliwashirikisha nia yetu ya kusafiri na kuwaomba watuombee. Na hapo tulikuwa na amani ya kuanza safari yetu.
Tulipofika kule Afrika Kusini tulikutana na yule daktari, na mara tulianza vipimo sote wawili, yaani mimi na mume wangu. Katika vipimo vile ilionekana
mimi nina vivimbe kwenye kizazi na nilihitaji kufanyiwa operesheni ya kuviondoa. Mume wangu na mimi tulikubali operesheni ifanyike. Tuliwashirikisha pia waombaji wenzetu pamoja na wazazi ili waendelee kutuombea.
Miezi saba baada ya operesheni ile, Mungu alinijalia nikapata ujauzito kwa mara ya kwanza, miaka 15 baada ya kufunga ndoa. Tulipogundua hilo tuliwasiliana na daktari wetu, na akanishauri nipate mapumziko hadi nijifungue. Nilifanya hivyo, na ninamshukuru Mungu leo hii nina mtoto wa kiume aitwaye Gift. Maana huyu ni zawadi toka kwa Mungu. Katika ushuhuda wangu huu nataka nikutie moyo wewe ambaye unapitia magumu. Mungu yupo, na hajawahi kushindwa. Uendelee kumtegemea na kuamini anaweza. Usikubali shida ikutoe katika kumpenda, kumtegemea na kumwishia Kristo.
Bertha Chris
Je, Mkristo anaweza kulaaniwa?
Mwafrika amefanya utafiti wa kina juu ya suala hili linalowaka moto, kisha amechunguza Biblia inasema nini.
Soma ujumbe wake mwema!
Kitabu hiki kinakupa kufuatana na Yesu dakika kwa dakika kipindi cha Pasaka, ukishuhudia jinsi alivyojitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote.
“Bwana amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, na kuwaacha huru waliosetwa.”
Ndivyo Yesu alivyojitambulisha. Ndivyo anavyofanya pia.
RIZIKI TOLEO 1, 2025
Mpendwa Msomaji wa RIZIKI
Tunatumaini umefurahi kusoma gazeti letu, na kwamba unataka kuendelea kulipokea.
Ili tuweze kuhakikisha hiyo, na kutolipeleka sehemu nyingine litakapolala tu na hatimaye kutupwa, tunaomba utusaidie kwa kutuma ujumbe mfupi kwa namba hii ya simu, +255 759 544 917, au kwa baruapepe hii, editor.somabiblia@gmail.com
Andika 1) Jina lako, 2) Anuani yako ya posta (kama unayo), 3) Njia unayotaka kutumiwa gazeti. Chagua njia moja kati ya hizi nne: a) baruapepe (kumbuka kujulisha jina lake), b) posta, c) dukani kwa Soma Biblia (kumbuka kujulisha mji gani) au d) ofisi au mtu fulani (kumbuka kujulisha jina).
Hata kama umepokea Riziki dukani kwetu au kupitia ofisi ya kanisa au mtu fulani, tafadhali tuma maelezo yako!
Asante, Kamati ya Rikizi
SOMA BIBLIA
0759 544 917
S.L.P. 2696, Arusha editor.somabiblia@gmail.com www.somabiblia.or.tz